Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Rais mstaafu Dk. Jakaya Kikwete, amesema atatumia uwezo na vipaji vyake kuhakikisha chuo hicho kinaendelea kuwa bora na kinatoa viongozi wa taifa.
Dk Kikwete aliyasema hayo juzi mara baada ya kumaliza kutembelea miradi mbalimbali ya maendeleo chuo hicho.
Miradi ambayo ameitembelea Dk. Kikwete ni pamoja na kituo cha mafunzo ya elimu, jengo la sayansi, eneo la maegesho na jengo la mihadhara la Yombo ambalo lina eneo la maktaba mpya.
Alisema changamoto ambazo zinakikabili chuo hicho nazo atazifanyia kazi kutokana na kuwa na uzoefu katika serikali kwa miaka mingi.
Aliongeza kuwa atapitia taratibu kwa kuisoma taarifa iliyotolewa na Makamu Mkuu wa Chuo, Profesa Rwekeza Mukandara, kisha kuitolea majibu kipindi ambacho watakutana tena mwishoni mwa mwezi huu.
Dk. Kikwete alipongeza uongozi wa chuo hicho kwa kuboresha miundombinu ambayo imekuwa kichocheo cha kuongezeka kwa wanafunzi.
Pia alimshukuru Rais Dk. John Magufuli kwa kumwamini na kumteua kwa kuwa mkuu wa chuo.
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment