dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Friday, December 9, 2016

NEC yawapa masharti CUF!

Dar/Dodoma. Wakati CUF ikijiandaa kushiriki uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Dimani, Zanzibar, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema fomu za wagombea wa chama hicho zitatakiwa kusainiwa na pande mbili zilizo na mgogoro wa uongozi.

Uamuzi huo mpya unaweza kusababisha chama hicho kukosa mgombea, hasa baada ya pande hizo baina ya Mwenyekiti Profesa Ibrahimu Lipumba anayetambuliwa na ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini na Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad kuendelea kuvutana huku kila upande ukijiandaa kivyake kwa uchaguzi huo.

Wakati hayo yakielezwa hivyo, jana Maalim Seif na timu yake walikutana na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kubadilishana taarifa juu ya hali ya kisiasa nchini na jinsi ya kushiriki katika uchaguzi huo kama Ukawa. Wengine waliohudhuria mazungumzo hayo ni Julius Mtatiro, Kingunge Ngombale Mwiru na Juju Danda wa NCCR-Mageuzi.Uchaguzi wa Dimani utafanyika Januari 22, 2017 kutokana na kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Hafidh Ally Tahir kilichotokea Novemba 11, mwaka huu katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma.

Baada ya uchaguzi huo kutangazwa na NEC, kila upande katika mgogoro huo ulianza kujiandaa, hali iliyoashiria kila upande kuibuka na mgombea wake.

Akiwa Dodoma jana, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Ramadhani Kailima alisema kutokana na CUF kuwa na mgogoro, mgombea atakayependekezwa atatakiwa kupitisha fomu zake na kusainiwa na viongozi wote wawili wa chama hicho wanaotambulika na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa.

“Kipengele cha 4(5) (iii) cha Sheria ya uchaguzi kinataka fomu za wagombea kwenye chama chenye mgogoro zisainiwe na viongozi wakuu wote wawili kwa vile wamethibitishwa na Msajili wa Vyama vya Siasa,” alisema.

Pia, tume hiyo ilisema wagombea pekee ama wawakilishi wao ndiyo watatakiwa kufanya kampeni katika eneo husika kwenye uchaguzi huo.

Hata hivyo, akizungumzia uamuzi huo, Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Nassor Ahmed Mazrui alieleza kustushwa na hatua hiyo na kusema: “Hii ni njia ya kutuondoa katika uchaguzi huu. Kwa sababu kwenye uchaguzi hakuna pande mbili, huwa moja,” alisema.

Mazrui alisisitiza kuwa hiyo ni njia ya kuiondoa CUF, lakini Ukawa itakuwapo na Baraza Kuu la Uongozi ndilo linateua mgombea.

“Kwa sasa siwezi kuzungumza chochote nitalipeleka kwa viongozi wenzangu kwa majadiliano zaidi,” alieleza Mazrui.

Hata hivyo, Mazrui alisema chama hicho kitashiriki kikamilifu na wana uhakika watashinda bila kikwazo chochote.

“Viongozi wa ngazi ya jimbo wameshaanza kutoa fomu kwa wagombea walionyesha nia ya kugombea. Nimeelezwa ni wengi waliojitokeza,” alisema Mazrui.

Aliongeza kuwa: “CUF ushindi upo pale hatuna wasiwasi na hilo. Ila tunataka uchaguzi uwe wa haki, huru na uwazi. Kinyume cha hapo hatutokubali,” alisisitiza Mazrui.

Mazrui alisema kuwa kuna ‘figisufigisu’ ambazo hakuwa tayari kuzitaja zimeshaanza kufanyika dhidi ya wanachama wao, lakini hawatarudi nyuma.

Wakati Mazrui akisema hayo, Naibu Katibu Mkuu wa CUF Bara, Magdalena Sakaya alisema taarifa hizo mpya za NEC zitawachanganya wanachama wao.

Alifafanua kuwa ngazi ya udiwani hakuna matatizo kwa sababu fomu zinasainiwa na katibu wa wilaya husika na haihusiani na katibu mkuu wala mwenyekiti; tofauti na ubunge ambapo jina la mgombea linajadiliwa na kupitishwa na Baraza Kuu linaloongozwa na mwenyekiti na katibu mkuu.

Mikutano ya siasa


Katika hatua nyingine, Kailima alisema kumekuwa na maswali mengi juu ya agizo la Serikali kupiga marufuku mikutano ya vyama vya siasa na kuruhusu ya kampeni kwenye maeneo yatakayofanya uchaguzi.

“Haturuhusu mgombea yoyote kufanya nje ya eneo analogombea, lakini pia haturuhusu chama chochote kinachogombea kutumia nafasi hii kufanya kampeni iliyo nje ya uchaguzi huu, kinyume cha hapo sheria zitachukua nafasi,” alisema.

Alisema chama kitakachokiuka mambo hayo kitapelekwa kwenye kamati ya maadili ya uchaguzi ili kichukuliwe hatua zaidi.

“Tume itaruhusu mkutano wa kampeni kwenye jimbo husika na chama husika na kwenye kata ama jimbo ni mgombea atakayeteuliwa na chama ama mwakilishi wake,” alisema Kailima.

Gharama za uchaguzi


Kailima alisema uchaguzi katika Jimbo la Dimani utagharimu Sh1.7 bilioni wakati katika kata 22 zitagharimu Sh2.2 bilioni.

CCM yafurahia

Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Vuai Ali Vuai alisema: “Kwanza nimefurahi sana kusikia CUF wanashiriki. Nawapongeza, hii demokrasia siyo kususa.”

Alisema hadi jana wanachama 12 wa CCM wamejitokeza kuchukua fomu za kuomba kuteuliwa kugombea ubunge wa jimbo hilo.

Alisema hadi kufikia leo zimebaki siku mbili kabla ya mchakato huo wa kuchukua fomu kufungwa rasmi ili hatua zingine zifuate, ikiwamo vikao vya kura za maoni.

“Desemba 11 watapigiwa kura za awali za maoni na wajumbe na mabalozi wa wilaya ya Dimani na Desemba 12 kamati ya siasa ya Dimani itatoa mapendekezo yake.

“Desemba 13 Kamati Maalumu ya Halmashauri Kuu ya CCM Zanzibar itakutana chini mwenyekiti, Dk Ali Mohamed Shein ili kufanya mchakato kwa kutangaza jina la mgombea,” alisema.

Alisisitiza ushindi upo palepale kwa CCM na kuwataka waliojitokeza kuchukua fomu ndani ya chama hicho kukubali matokeo ya uteuzi.

No comments :

Post a Comment